Sunday, November 25, 2012

Jinzi ya Kujikomboa Kimasha Kwa Vijana

SINA shaka kuna watu wametafuta sana elimu, kazi, biashara, wachumba, watoto, uongozi na mambo mengine mengi waliyoyahitaji katika maisha yao na kwa kiwango chao wamepata. Lakini tathmini inaonesha kuwa, asilimia 87 ya watu waliopata walivyokuwa wanatafuta hawanufaiki navyo au kwa lugha nyingine kupata kwao hakukuwasaidia. Mamia kwa mamia ya vijana wametumia au wanatumia mpaka sasa karibu nusu ya maisha yao kutafuta elimu, lakini wanapoipata haiwasaidii wao kama watafutaji, haiwanufaishi wazazi na walezi na haina tija pia hata kwa taifa lao. Huo ni mfano mmoja, lakini wapo watu wanaotumia muda mwingi kutafuta wasichana wazuri wa kuoa, wanatumia muda mwingi kutafuta fedha, wanajituma kupita katika maofisi na vyeti vyao asubuhi na jioni kutafuta kazi, wakiamini kuwa wakipata wanavyotafuta watanufaika. Lakini kupata kunapotokea ni wachache wanaoonesha mabadiliko waliyotarajia wao wenyewe au jamii walizotoka na wanazoishi! Ni mara ngapi tumeshuhudia wasomi wakifanya mambo ya ovyo pamoja na elimu zao? Au hatuwaoni watu wanachezea ajira kwa kutojali sheria za kazi, kuwa wazembe, wezi na hata mafisadi? Hii ina maana kwamba, vijana wengi walipozaliwa walifundishwa na wazazi wao kutafuta, ndiyo maana hakuna asiyejua njia za kutafuta na uthibitisho wa hili upo kwenye shughuli wanazojishughulisha nazo. Watoto wa wakulima wanajua kutafuta maisha kupitia kilimo, kwao ili kupata maisha ni kuwa hodari wa kushika jembe, kwa nini? Walifundishwa na wazazi wao tangu utotoni kutafuta kwa njia ya kilimo. Vivyo hivyo kwa wazazi wafanyabiashara, wasomi na hata viongozi. Kumbe tatizo la vijana wa leo si la kujua njia za kutafuta na kupata mahitaji yao tu bali ni pamoja na kuelewa namna ya kutumia vizuri vitu wanavyopata. Ni lazima vijana wajue namna ya kutumia fedha wanazopata bila kujali ni nyingi kiasi gani. Inawezekana nikisema kutumia fedha anazopata kuna wanaoweza kudhani nazungumzia mamilioni na hivyo wao wenye kipato cha shilingi 10,000 somo hili haliwahusu. Kimsingi kanuni sahihi ya matumizi ya fedha yoyote duniani, ili iweze kuleta mafanikio kwa mtumiaji bila kujali kiwango, ni INGIZA PESA NYINGI TUMIA CHACHE. Kwa bahati mbaya elimu hii vijana wengi hawapewi na wazazi wao, kwa maana hiyo hawajui namna ya kutumia vizuri fedha wanazopata na hapo ndipo wanapokutana na tatizo la mshahara hautoshi. Mbali na suala la fedha, vijana wengi kama nilivyosema hawafahamu namna ya kutumia vitu wanavyovitafuta na kuvipata. Leo tuna vijana wengi wanaoa, lakini hawajui kuwatumia wake zao, matokeo yake wanajikuta wakivutwa na tamaa za kwenda kwa wanawake wengine na kuangukia magonjwa, fumanizi au vishawishi vya kufanya mabadiliko ya wapenzi waliowachagua mwanzo. Yote hayo yanatokana na kutojua namna ya kutumia vitu, maana haijapata kutokea mtu akatosheka na anachopata, isipokuwa awe na elimu inayomuwezesha kutambua matumizi sahihi ya vitu anavyojikusanyia maishani mwake. Kwa msingi huo naamini kila anayesoma mada hii, ana vitu anavyomiliki, inaweza kuwa elimu, kazi, ujuzi, biashara, mali, nyumba, watoto, mke, mume na hata dini, lakini shaka yangu inabaki kwenye matumizi sahihi. Hebu tujiulize, tunazitumia vema dini zetu, tunawatumia vizuri waume zetu baada ya kuoana nao, tunawalea sawa sawa watoto tuliowatafuta kwa miaka mingi? Itaendelea wiki ijayo. Je, tunazitumia kazi tulizopata kwa moyo au tunafanya uzembe, tunaiba na kunyanyasa watu? Tulitafuta gari tukapata, tunalitumiaje gari hilo, je ni kama gesti ya kufanyia uhuni na wake za watu au ni kwa ajili ya kutusaidia katika shida za usafiri? Ni lazima tujifunze na kujua namna ya kutumia vema vitu tunavyopata ili tuweze kupata mafanikio. Kimsingi kutafuta pekee hakuwezi kubadilisha maisha ya vijana kama vitu vinavyopatikani havitumiwi kwa nidhamu. TUNAVYOPOTEZA Watu wengi wanatafuta vitu na kupata, lakini kuna jambo moja kubwa ambalo limekuwa likiwatokea nalo ni kupoteza walivyopata. Wapo waliotafuta kazi, fedha, nyumba, magari, wakapata lakini leo tunaposoma somo hili kupata kwao kumebaki historia. “Khaa! Huyu usimuone hivi amesoma sana, sema tu alipata matatizo. Jamaa alikuwa na maisha mazuri sana lakini ilitokea bahati mbaya akafilisika. ”Hizi ni baadhi ya kauli ambazo zimekuwa zikitolewa kuwahusu watu waliopata vitu fulani, lakini wakavipoteza. Kupoteza yaliyopatikana kuna sababu kuu mbili, nazo ni kupoteza kusikotarajiwa na kupoteza kwa matarajio. Ninaposema kusikokuwa na matarajio ninamaanisha majanga ambayo huwakuta watu bila wao wenyewe kuzembea mahali popote. Kwa mfano ukame, kimbunga, wizi, ajali na kadhalika. Ninapozungumzia kupoteza kwa matarajio ninamaanisha matukio yanayotokana na kuwepo kwa uzembe wa mtu mwenyewe katika kusimamia mambo aliyoyapata. Kwa mfano kupata utajiri na kuanza kufuja fedha kwa anasa, kuhonga, kutozingatia kanuni za kupata kingi na kutumia kichache na mambo kama hayo ni moja kati ya sababu za kizembe ambazo huwafanya vijana kama si watu wengi kupoteza walivyopata. Lakini pamoja na kuwepo kwa sababu hizo mbili za kupoteza, wataalamu wanasema watu wengi wanaotokewa na tatizo hili wanatoka katika kundi la pili, yaani wanaopoteza kwa makusudi. Uchunguzi unaonesha kuwa asilimia 91 ya wanaopoteza vitu walivyovipata wanajitakia, lakini ni asilimia 4.5 kati yao ndiyo wanaotambua baadaye kuwa kupoteza kwao kulitokana na wao wenyewe na asilimia zilizobaki huhifadhi makosa yao kwenye sababu ya kwanza yaani kupoteza kusikotarajiwa. Hii ina maana kuwa, ni watu wachache sana ambao wanatafuta na kupata kisha kupoteza na hatimaye kutafuta tena kwa mara ya pili na kupata pengine zaidi ya walivyopata mwanzo. Lakini wengi wao kama tulivyoona wakipoteza hushindwa kutafuta tena na kujikuta wakizama kwenye hali mbaya mpaka wanakufa au kujikuta wakipata vitu dhaifu sana. Ni vema wakati tunatafakari hili, tukajiuliza ni watu wangapi ambao tunawafahamu, walifukuzwa kazi, wakahangaika kupitia uzoefu na uwezo wao kupata kazi nyingine nzuri zaidi ya zile walizokuwa nao? Je, ni watu wangapi ambao biashara zao zikifilisika huanza mwanzo kutafuta mtaji na kufanikiwa kurudisha maduka yao kwa ukubwa ule ule au zaidi? Ni wangapi ambao, walipoteza wapenzi, wake/waume na hatimaye kupata wengine wazuri kiasi cha kusema wamepata bora kuliko wa kwanza? Bila shaka watakuwepo, lakini haiwezi kuwa idadi ya kuzidi asilimia 4.5 niliyoitaja hapo juu. Kama hali iko hivi ni wazi kwamba vijana wengi hawafahamu kanuni ya kutafuta baada ya kupoteza. Kwa kuwa hawafahamu hilo wengi wao wamejikuta wakifanya makosa na kuambulia madhara makubwa likiwemo suala la kukata tamaa ya kufanikiwa kimaisha

No comments:

Post a Comment